Monday 20 July 2015

WASANII WAIOMBA SERIKALI KUUMALIZIA UKUMBI WA BASATA


Na Mwandishi Wetu

Wasanii nchini wameiomba Serikali kumalizia ujenzi wa ukumbi wa Sanaa za maonesho unaojengwa kwa zaidi ya miaka minane sasa makao makuu ya Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) eneo la Ilala sharif Shamba jijini Dar es Salaam.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti kwenye programu ya Jukwaa la Sanaa ya Baraza hilo mapema wiki hii, wasanii hao walieleza kwamba kwa sasa kuna ufinyu wa kumbi za za maonesho hali ambayo imekuwa ikiwafanya wasanii hao kukosa maeneo ya kufanya sanaa zao hivyo kumalizika kwa ukumbi huo itakuwa ni ahueni kubwa kwao.

“Ukumbi huu ni muhimu sana kwetu, wengi tuliutazama kama mwanzo wa ufufuaji wa Sanaa za majukwaani lakini sasa ni muda mrefu hauoneshi dalili za kumalizika. Kuna kila sababu ya ukumbi huu kukamilika ili kutusaidia katika maonesho yetu” alisema Msanii Khalid Kambau.

Kwa upande wake msanii wa Sanaa za maigizo Christian Kauzeni ambaye pia ni mwenyekiti wa chama cha wasanii waigizaji mkoani Dar es Salaam alisema kwamba kutokana na ukumbi huo kutazamwa kama mkombozi wa wasanii kuna kila sababu ya kuangalia mbinu mbalimbali ili kuhakikisha unakamilika mapema iwezekanavyo.

Awali akiwasilisha mada kwenye Jukwaa hilo la Sanaa iliyohusu ‘Ubora wa Filamu na Changamoto zake’ msanii na mzalishaji filamu maarufu nchini William Mtitu alisema kwamba tasnia ya filamu chini imepata umaarufu na kukua ingawa bado changamoto za uharamia, elimu na masoko zimeendelea kuiathiri.

“Kwa sasa filamu zinazozalishwa zimekuwa na ubora kuliko huko nyuma. Tatizo liko kwenye elimu kwa wasanii, uharamia na masoko. Kulikuwa na maduka zaidi ya sabini na tano yanayouza kazi za wasanii wa filamu lakini kwa sasa yamebaki sita tu. Wengi wameamua kuuza kazi za nje mbazo ni nafuu. Hii ni hatari” alisisitiza Mtitu.  

Aliongeza kwamba pamoja na Serikali kuirasimisha sekta ya filamu bado kuna changamoto ya kazi zinazotoka nje kutokuwekewa stempu za mamlaka ya mapato huku kukiwa na uharamia unaotishia bei za filamu halali zenye stempu hizo.

Jukwaa la BASATA limekuwa likifanyika kwa mwezi mara mbili siku za Jumatatu na wiki hii kulikuwa pia na utambulisho wa asasi ya ubalozi wa Utamaduni wa Mwafrika ambayo imeasisiwa nchini Cameroon, Afrika Magharibi mwaka 2014.








 

No comments:

Post a Comment