Thursday 13 July 2017

TCRA YAHIMIZWA WASANII JUU YA MATUMIZI SAHIHI YA MITANDAO YA KIJAMII

Naibu Mkurugenzi - Masuala ya watumiaji wa huduma za mawasiliano kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Bw. Thadayo Joseph Jonas Ringo (katikati) akitoa elimu juu ya matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii katika ukumbi mdogo wa BASATA. Wengine ni Mkurugenzi wa fedha na utawala kutoka BASATA Bw. Onesmo Kayanda na Bi. Agnes Kimwaga (Afisa Habari Mkuu - BASATA).
Kupitia programu ya "Jukwaa la Sanaa" inayo ratibiwa na Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) ambayo hufanywa kila wiki, wasanii mbalimbali jana waliudhuria ili kuweza kufahamu faida na madhara juu ya mitandao ya jamii. Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) walitoa elimu kwa wasanii juu matumizi sahii ya mitandao ya kijamii hasa katika zama hizi za sayansi na teknolojia.

Akieleza hayo katika ukumbi mdogo wa BASATA uliopo Ilala Shariff Shamba  muwakilishi kutoka TCRA Bw. Thadayo Joseph Jonas Ringo alisema..
"mitandao ya kijamii itakupa jina, umarufu na faida nyingi sana katika jamii kama ikitumika vizuri kwa malengo yaliyokusudiwa.., na kwa hakika utaifurahia sana. Lakini pia mitandao hii inakuwa kama shubiri iwapo tutaitumia vibaya kwa malengo ya kiudanganyifu, kuwachafua watu ama kuweka picha zako chafu."
Bw. Ringo akaendelea.
"Na asikudanganye mtu kuwa ukivunja sheria kwa kudanganya jina lako kwenye mtandao eti hatuwezi kukupata, kwa kushirikiana na mamlaka nyingine tutakupata tuu kwa namna yoyote ile, hivi mnajua kuwa mtu akiingia kwenye mtandao (internet) kuna alama zaidi ya elfu moja huwa anaziacha pale!? Hivyo utapatikana tuu na utafikishwa kwenye vyombo vya sheria."

Pamoja na kutoa tahadhari hiyo, bwana Ringo aliendelea kuuelimisha umma wa Watanzania kupitia wasanii kuwa huduma za mitandao ya kijamii ikiwemo simu na kompyuta ni muhimu katika matumizi yetu ya kila siku kimawasiliano, hivyo ingawa teknolojia hii ni mpya na inaendelea kukua aliwataka watumiaji kuzingatia matumizi bora na kufuata sheria za kimtandao.

Pia aliwakumbusha Watanzania kuwa ni muhimu sana kutoa taarifa polisi mara tu utakapoteza simu, kompyuta, laini ya simu ama kifaa chochote ambacho kimebeba taarifa zako ili uweze kujiweka katika mazingira salama kwa lolote litakaloweza kutokea.

Aliongelea pia kuhusu wadukuzi wa akaunti za watu kuwa ni muhimu pia kutoa taarifa mapema kwenye mamlaka husika iwapo akaunti yako unayoitumia kwenye mitandao ya kijamii imeporwa na mtu mwingine. Alimalizia bwana Ringo.

Katibu wa chama cha Ma DJ Tanzania bwana Asanterabi Mtaki (aliyesimama) akitoa ufafanuzi juu ya jambo fulani.
Mwandishi Bwana Ali Thabiti na wenzake wakimhoji mtoa mada Bw.Ringo
Sehemu ya umati wa wasanii mbalimbali waliohudhuria progamu ya Jukwaa la Sanaa mapema jana BASATA

No comments:

Post a Comment