Thursday 18 June 2015

JUKWAA LA SANAA

BASATA LAWATAKA WASANII KUWA TAYARI KUKOSOLEWA

Na Mwandishi Wetu

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limetoa wito kwa wasanii kuacha tabia ya kulewa umaarufu na kuchukia pale wanapokosolewa kwani kazi yoyote ya Sanaa lazima ikosolewe ili iwe bora na yenye kuvutia.

Wito huo umetolewa mapema wiki hii na Katibu Mtendaji wa Baraza hilo Godfrey Lebejo Mngereza wakati akizungumza kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA linalofanyika kwa mwezi mara mbili siku ya Jumatatu kwenye Ukumbi wa Baraza hilo ulioko Ilala Sharif Shamba jijini Dar es Salaam.

Alisema kuwa wasanii wafurahie wanapokosolewa kwani msanii yeyote duniani lazima atenge muda wa kuiwasilisha kazi yake kwa hadhira kwa ajili ya kusikilizwa au kuangaliwa na hatimaye kukosolewa na kutolewa mawazo ya wadau kabla haijaenda sokoni rasmi.
“Kukosolewa kwa msanii ni sehemu ya kazi. Wasanii wengine hulipa fedha nyingi kwa ajili ya kukosolewa na kuboreshewa kazi zao. Hapa kwetu wasanii wanakosolewa bure, wanakasirika, wanamwona adui anayewakosoa” aliongeza Lebejo.

Awali wakiwasilisha mada iliyohusu Umuhimu wa msanii kutumia umaarufu kukuza pato kwa nyakati tofauti kwenye Jukwaa hilo, mbunifu wa mavazi maarufu nchini Asia Idarous and mwanamitindo Jokate Mwegelo kwa pamoja walisisitiza umuhimu wa wasanii kuwa na malengo, bidii, uaminifu na kutengeneza kazi zenye ubora.

Jokate alisema kwamba amefika hapo alipo kutokana na kuzingatia uhusiano mwema katika kazi, kujitangaza, kujituma, kujiwekea akiba na kujenga mtandao mzuri wa kikazi na wadau mbalimbali ndani na nje ya nchi pia kujenga umaarufu mzuri usiyo na maadili mabovu.

“Kupata umaarufu si kwa mteremko. Si kila umaarufu ni mzuri. Wasanii lazima wabuni kazi nzuri na zenye maadili ili zionekane na kupendwa. Tusibuni vitu vibaya au sisi wenyewe kujinadi kwa vitu vibaya” alisisitiza Jokate.

Alizidi kueleza kwamba hakuna kitu cha muhimu kwa msanii kama uvumilivu , kuepuka makundi yasiyo na tija na zaidi kuwa karibu na watu wenye mafanikio katika kazi zao ili kuiga yale yaliyo bora kwa ajili ya kukuza uchumi na pato.  




Habari katika picha.








No comments:

Post a Comment