Tuesday 30 June 2015

WASANII WAOMBA KUPUNGUZIWA KODI KWENYE VIFAA VYA MUZIKI

Na Mwandishi Wetu
Baadhi ya wasanii nchini wameiomba Serikali kupitia Wizara ya Fedha kufikiria kupunguza au kufuta kabisa ushuru wa forodha unaotozwa kwenye vifaa vya muziki wanavyoagiza kutoka nje ili kukuza Sanaa na kusaidia mamilioni ya vijana ambao wamejiajiri kupitia sekta hiyo.

Akizungumza kwa niaba ya wasanii mapema wiki hii kwenye Jukwaa la Sanaa la Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) mmoja wa wasanii anayeunda kundi la muziki wa kizazi kipya la Weusi Nick wa Pili alisema kwamba, kwa sasa sekta hiyo ni kimbilio la ajira kwa vijana wengi kwa hiyo Serikali haina budi kupunguza kodi kwa zana mbalimbali zinazotumiwa na wasanii ili kurahisisha uzalishaji, kukuza tija na uchumi.

“Wasanii wengi kwa sasa wanakwenda kufanya video na kutengeneza muziki nje ya nchi. Hii inatokana na teknolojia yetu kuwa chini ya wenzetu. Naamini Serikali ikipunguza kodi katika vifaa hivi na kuwawezesha wataalam tulionao basi nchi zote jirani zitakimbilia kwetu” alisema Nick

Aliongeza kwamba vipaji vya wasanii vipo vingi lakini kutokana na uzalishaji duni wa kazi za muziki na hata filamu wasanii wamejikuta wakishindwa kushindana ipasavyo nje ya nchi na mara nyingi kutumia gharama kubwa katika kufuata teknolojia hizo za juu nchi za nje na hivyo kuikosesha serikali mapato.

“Wasanii wanakwenda kulipa zaidi ya milioni arobaini kwa video moja tu nje ya nchi, hizi fedha zinakwenda kukuza uchumi wa nchi zingine. Naamini kama Serikali ikijenga mazingira mazuri ya kiteknolojia na zaidi kushusha gharama hizi basi nchi yetu itafaidika zaidi na Sanaa” alizidi kusisitiza Nick.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Mitaji na Misaada kwa wasanii kutoka BASATA Bi. Elineca Ndowo alisema kwamba sekta ya Sanaa nchini inazidi kukua na hivyo lazima wasanii nao wafikirie kufanya kazi kisasa na kwa kufuata taratibu zote ili kuipa serikali uhakika katika kupanga kulingana na hali halisi.

“Sekta ya Sanaa inakua, lazima tuisaidie Serikali kuipa takwimu sahihi na moja ya njia ya kuhakikisha hili ni kwa wasanii kujisajili, kusajili kazi zao na kuhakikisha taarifa sahihi na kwa wakati zinapatikana. Hili litarahisisha upangaji wa mipango” alisema Bi. Ndowo.

Jukwaa la Sanaa la BASATA ni programu ambayo hufanyika kwa mwezi mara mbili siku ya Jumatatu na hutumika kama jamvi la kuwaelimisha wasanii na kuwakutanisha kwa pamoja katika kubadilishana uzoefu na mawazo kuhusu masuala mbalimbali yahusuyo sekta yao.  


     Msanii wa muziki wa kizazi kipya kutoka Kundi la Weusi Nick wa Pili (Kushoto) akisisitiza jambo wakati akiongea na wadau wa Sanaa (hawako pichani) kwenye programu ya Jukwaa la Sanaa inayofanyika kwa mwezi mara mbili siku ya Jumatatu makao makuu ya Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) Ilala Sharif Shamba jijini Dar es Salaam. Wengine kushoto kwake ni wasanii wanaounda kundi hilo John Simon aka Joh Makini na G Nako na Afisa kutoka BASATA Bi. Elineca Ndowo. 



      Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Mitaji na Misaada kwa wasanii kutoka Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) Bi. Elineca Ndowo (Kulia) akiongea na wadau wa Sanaa (hawako pichani) kuhusu masuala mbalimbali kwenye programu ya Jukwaa la Sanaa ambayo huandaliwa kwa mwezi mara mbili ziku ya Jumatatu na Baraza hilo. Wengine katika picha kulia kwake ni Wasanii G Nako na John Simon maarufu kama Joh Makini wanaounda kundi la muziki wa kizazi kipya la Weusi. 



     Msanii G Nako kutoka Kundi la muziki wa kizazi kipya la Weusi akiimba sambamba na msanii mchanga ambaye hakufahamika mara moja kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA mapema wiki hii. 



     Mdau huyu wa Sanaa naye hakuwa nyuma. Aliuliza sababu za Wasanii wengi wa kizazi kipya kupenda kutumia playbacks badala ya kuimba live Jukwaani.



    Msanii anayechipukia kwenye tasnia ya filamu kutoka taasisi ya mafunzo ya TAMAP akiwauliza maswali mbalimbali wasanii wa kundi la Weusi kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA mapema wiki hii.












Picha, habari na Aristides Kwizela, Afisa Habari wa BASATA.

Thursday 18 June 2015




TANGAZO KWA WASANII WOTE

YAH: MWALIKO WA KUSHIRIKI TAMASHA LA UTAMADUNI JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI JAMAFEST – 2015

Tafadhali rejea kichwa cha habari hapo juu.

Baraza la Sanaa la Taifa limepokea taarifa ya mwaliko kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kuwa Tamasha la Utamaduni la Jumuiya ya Afrika Mashariki linatarajiwa kufanyika nchini Kenya, jijini Nairobi, kwa siku 8 kuanzia tarehe 2 – 9 Agosti, 2015.

Tamasha hili litahusisha mambo mbalimbali ikiwemo Sanaa za jukwaani, Maonesho ya bidhaa mbalimbali za Kiutamaduni, Warsha na kongamano, Michezo na Sanaa za Watoto, Kutembelea vivutio asilia na vya Utamaduni na Soko la Tamasha la kuuzia bidhaa za kiutamaduni.

Baraza linahimiza vikundi, vyama na mashirikisho ya sanaa, wasanii na wadau wa sanaa kutumia fursa hii kuonesha kazi bora za sanaa za Kitanzania.

Aidha, washiriki watapaswa kujigharamia usafiri wa kwenda na kurudi hadi Nairobi, Malazi, chakula wakati wote wa Tamasha, tiba na bima.

Kwa maelezo zaidi unaombwa kufika Ofisi za BASATA, Idara ya Ukuzaji Sanaa na Masoko au piga simu namba 0789 094 477

Nakutakia maandalizi mema.

Godfrey L. Mngereza
KATIBU MTENDAJI



Barua zote ziandikwe kwa Katibu Mtendaji
All correspondence to be addressed to The Executive Secretary
BASATA Arts Centre, Ilala Sharif Shamba, P.O. Box. 4779, Dar es Salaam, Tanzania.
Telephone: 2863748/2860485, Fax: 0255 – (022) 286 0486 E-mail: basata06@yahoo.com Website: basata.or.tz


JUKWAA LA SANAA

BASATA LAWATAKA WASANII KUWA TAYARI KUKOSOLEWA

Na Mwandishi Wetu

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limetoa wito kwa wasanii kuacha tabia ya kulewa umaarufu na kuchukia pale wanapokosolewa kwani kazi yoyote ya Sanaa lazima ikosolewe ili iwe bora na yenye kuvutia.

Wito huo umetolewa mapema wiki hii na Katibu Mtendaji wa Baraza hilo Godfrey Lebejo Mngereza wakati akizungumza kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA linalofanyika kwa mwezi mara mbili siku ya Jumatatu kwenye Ukumbi wa Baraza hilo ulioko Ilala Sharif Shamba jijini Dar es Salaam.

Alisema kuwa wasanii wafurahie wanapokosolewa kwani msanii yeyote duniani lazima atenge muda wa kuiwasilisha kazi yake kwa hadhira kwa ajili ya kusikilizwa au kuangaliwa na hatimaye kukosolewa na kutolewa mawazo ya wadau kabla haijaenda sokoni rasmi.
“Kukosolewa kwa msanii ni sehemu ya kazi. Wasanii wengine hulipa fedha nyingi kwa ajili ya kukosolewa na kuboreshewa kazi zao. Hapa kwetu wasanii wanakosolewa bure, wanakasirika, wanamwona adui anayewakosoa” aliongeza Lebejo.

Awali wakiwasilisha mada iliyohusu Umuhimu wa msanii kutumia umaarufu kukuza pato kwa nyakati tofauti kwenye Jukwaa hilo, mbunifu wa mavazi maarufu nchini Asia Idarous and mwanamitindo Jokate Mwegelo kwa pamoja walisisitiza umuhimu wa wasanii kuwa na malengo, bidii, uaminifu na kutengeneza kazi zenye ubora.

Jokate alisema kwamba amefika hapo alipo kutokana na kuzingatia uhusiano mwema katika kazi, kujitangaza, kujituma, kujiwekea akiba na kujenga mtandao mzuri wa kikazi na wadau mbalimbali ndani na nje ya nchi pia kujenga umaarufu mzuri usiyo na maadili mabovu.

“Kupata umaarufu si kwa mteremko. Si kila umaarufu ni mzuri. Wasanii lazima wabuni kazi nzuri na zenye maadili ili zionekane na kupendwa. Tusibuni vitu vibaya au sisi wenyewe kujinadi kwa vitu vibaya” alisisitiza Jokate.

Alizidi kueleza kwamba hakuna kitu cha muhimu kwa msanii kama uvumilivu , kuepuka makundi yasiyo na tija na zaidi kuwa karibu na watu wenye mafanikio katika kazi zao ili kuiga yale yaliyo bora kwa ajili ya kukuza uchumi na pato.  




Habari katika picha.